Jumatatu, 24 Novemba 2014

IRINGA YAJIVUNIA USAFI WA MAZINGIRA



 Vijana wa kikundi cha usafi na uhifadhi wa mazingira cha Umoja wa vijana wazalendo Mbeya(UVIWAMBE), kutoka Mbalizi Mbeya, wakiwa katika picha ya pamoja mjini Iringa wakati wa ziara yao ya mafunzo.
HALMASHAURI ya Manispaa ya Iringa, imesema inajivunia kuwa ni moja ya Halmashauri zenye mazingira safi nchini, kutokana na juhudi za uelimishaji wananchi wake, ikiwa ni pamoja na kutumia vyombo vya habari.

Hayo yalielezwa juzi katika ukumbi wa mikutano wa Manispaa hiyo na Afisa Afya wa Manispaa hiyo, Christian Ndenga, alipokuwa akitoa taarifa ya maarifa wanayoyatumia kuweka mji safi, alipotembelewa na kikundi cha usafi na uhifadhi wa mazingira cha Vijana wazalendo Mbeya(UVIWAMBE), kutoka wilaya ya Mbeya Vijijini, mkoani Mbeya.

Ndenga alisema kuwa, manispaa hiyo imepata tuzo ya mshindi namba moja kuhusu usafi wa mji, kutokana na jitihada kubwa zinazofanywa baina ya serikali, vikundi vya usafi na wadau wengine wakiwemo wafanyabiashara.

“Tunajivunia mafanikio haya kutokana na kwanza kuwepo kwa sheria zinazodhibiti wachafuzi wa mazingira ambao hutozwa faini isiyozidi Shilingi Elfu Hamsini, kukasimu madaraka ya masuala ya usafi ngazi za kata, uwepo wa vikundi vya usafi na kutosubiri makontena ya uchafu yajae ndipo yakamwagwe” alisema Ndenga.

Alitaja pia vyombo vingine wanavyotumia ili kuhakikisha mji unakuwa safi kuwa ni pamoja na kuwatumia viongozi wa dini, shule na vyuo, huku akisema kuwa waandishi wa habari wamekuwa mstari wa mbele kufika katika ofisi za manispaa kuhoji kama kuna sehemu wameona uchafu jambo ambalo alisema kuwa linawapa msukumo wa kufanya vizuri zaidi na kutoa elimu kwa wananchi.

Alisema kwa sasa, wanapanga mpango wa miaka 20 ijayo kuandaa eneo la kutupia taka badala ya kusubiri eneo walilonalo kwa sasa mpaka hapo litakapojaa.

Baada ya taarifa hiyo, kikundi cha Uviwmbe waliongoza na afisa mmoja wa Manispaa hiyo kitengo cha Afya, Ezekiel Mbushi, kwenda kutembelea soko la Iringa mjini na kukutana na uongozi wa kikundi cha usafi cha mjini hapo kijulikanacho kwa jina la Kikundi cha wafanyabiashara wa masoko(KWBS).

Mwenyekiti wa kikundi hicho Augustino Ngao na katibu wake Aldo Kaduma, walisema kuwa, ili wananchi waweze kutii sheria za usafi ni muhimu wakapatiwa elimu kwanza kabla sheria haijaanza kufanya kazi ambapo walikiri kuwa pamoja na baadhi kupata elimu katika manispaa hiyo, lakini bado wanakuwepo wanaokaidi.

“Changamoto tunayopata katika kutekeleza kazi za usafi ni pamoja na baadhi kukaidi kutii sheria, watu wa haki za binadamu kutukamata wanapowakuta baadhi ya vibarua wa kikundi wakifanya kazi bila kuvaa grovu na pia vifaa kuwa duni yakiwemo matolori ambayo ni tofauti na yale yaliyokuwa yakitengenezwa Mbeya na kiwanda cha ZZK ambacho kilikufa” alisema Kaduma.

Mwanasheria wa Halmashauri ya Mbeya, Prosper Msivala, ambaye aliongozana na wana kikundi cha Uviwambe, alisema kuwa yeye alikuwa mwanasheria wa Manispaa ya Iringa na ni mzawa wa mkoa huo, ambapo anaikumbuka historia mbaya ambayo iliwezesha manispaa hiyo kufika hapo ilipo kuhusu suala la usafi.

“Hapa Iringa mwaka 1988, kulitokea mlipuko wa kipindupindu ambapo kwa siku zaidi ya wananchi 50 walikuwa wakifa na kuzikwa, jambo ambalo lilihamasisha jamii nzima kuanza kuzingatia suala la usafi na kuna wakati tulifikia mahala tukavunja vibanda vilivyowekwa kiholela na baadhi ya nyumba na tukatishiwa kuuawa, lakini kwa sasa mambo safi” alisema Msivala.

Mwenyekiti wa kikundi cha Uviwambe, Ayas Yusuph, aliishukuru Halmashauri ya Mbeya kwa kugharamia safari hiyo na Manispaa ya Iringa kwa kuwapa elimu na kuwaunganisha na kikundi cha usafi cha KWBS na kwamba elimu na maarifa waliyopata katika ziara hiyo ya mafunzo wataitumia vema.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

NAIBU WAZIRI WA KILIMO MHE MWANJELWA AMUAGIZA MRAJIS KUFANYA UCHUNGUZI SACCOS YA MADIBIRA-MBARALI NDANI YA SIKU 14

Naibu Waziri wa Wizara ya Kilimo, Mhe Mary Mwanjelwa akisisitiza jambo wakati akizungumza na Viongozi mbalimbali wa Mkoa na kamati ya uli...