Jumapili, 21 Septemba 2014

KITUO CHA AFYA CHA AGA KHAN CHATOA MSAADA WA VIFAA TIBA

 
MKUU WA MKOA WA MBEYA ABBAS KANDORO
 
KITUO cha afya cha Aga khan, tawi la Mbeya, kimetoa msaada wa vifaa tiba katika Hospitali na vituo vya afya katika Halmashauri 4 za Mkoa wa Mbeya vyenye thamani ya zaidi ya shilingi Milioni 300.
 
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro kwa niaba ya Halmashauri husika, alipokea msaada huo katika ukumbi wa Mkapa uliopo jijini Mbeya.
 
Mratibu wa Mradi wa tuunganishe mkono pamoja(JHI) Mkoa wa Mbeya, Abel Kide, ambaye pia ni Meneja wa Hospitali ya Aga Khan alisema Halmashauri zilizonufaika na mradi huo ni Jiji la Mbeya, Kyela, Mbozi na Momba.
 
Alizitaja Hospitali na zahanati zinazopatiwa vifaa hivyo kuwa ni Zahanati ya Ngana na Hospitali ya Wilaya ya Kyela(Kyela), Zahanati ya Iyunga na kituo cha Afya Kiwanja Mpaka(Mbeya jiji), Hospitali ya Wilaya ya Mbozi(Vwawa)na Zahanati ya Ivuna iliyopo wilayani Momba.
 
Alivitaja vifaa hivyo kuwa ni Vitanda vya kujifungulia wajawazito, vitanda vya wagonjwa wa kawaida, Mashine za kuchemshia vifaa vya hospitalini, Mashine ya kumpa joto mtoto aliyetoka kuzaliwa, Mashine ya Ultra Sound,Mashine ya kumtolea uchafu mtoto mchanga,mashine za kupima uzito, joto, urefu na Presha na kwamba vyote jumla vinagharimu zaidi ya shilingi Milioni 300.
 
Lengo la msaada huo ni kuboresha afya ya mama mjamzito, mtoto mchanga na mtoto aliye chini ya miaka mitano ikiwa ni pamoja na kusogeza huduma za afya  karibu na wananchi hususani kuokoa vifo vinavyotokea wakati wa kujifungua.
 
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbasi Kandoro alipongeza Hospitali ya Aga Khan kwa Msaada waliotoa katika Halmashauri hizo na kuziomba taasisi zingine kuungana na Serikali katika mpango wa kuhakikisha vifo vya Wanawake wajawazito, watoto wachanga na walio chini ya umri wa miaka mitano vinapungua.
 
Aliongeza kuwa ili kukomesha kabisa vifo hivyo, Halmashauri zitenge bajeti za kununua mfumo wa huduma tembezi(Mobile clinic) ili ziweze kufika hata maeneo ambayo hakuna huduma ya afya kwa kuwasogezea wananchi huduma ili waweze kupata msaada wa matibabu wakati wowote.
 
Sambamba na kupokea msaada huo Mkuu wa Mkoa wa Mbeya alizindua Mpango wa utekelezaji wa kupunguza kasi ya vifo vitokanavyo na matatizo ya uzazi, watoto na watoto waliochini ya umri wa miaka mitano.
 
Kandoro aliongeza kuwa mkakati huo ni maagizo ya Raisi wakati wa uzinduzi wa kitabu cha Mkakati wa kitaifa uliofanyika Mei 15 Mwaka huu ambapo aliagiza Kila Mkuu wa Mkoa kuutafakari mkakati huo kulingana na mazingira wanakotoka.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

NAIBU WAZIRI WA KILIMO MHE MWANJELWA AMUAGIZA MRAJIS KUFANYA UCHUNGUZI SACCOS YA MADIBIRA-MBARALI NDANI YA SIKU 14

Naibu Waziri wa Wizara ya Kilimo, Mhe Mary Mwanjelwa akisisitiza jambo wakati akizungumza na Viongozi mbalimbali wa Mkoa na kamati ya uli...