Ijumaa, 17 Januari 2014

WAZAZI WAPINGA KULAZIMSHWA WATOTO WAO KUJIUNGA NA ELIMU YA WATU WAZIMA



 Wananchi wakisikitika kutokana na majibu ya wakubwa....
 Baadhi ya wazazi wakiwa wanaangalia majina ya watoto wao, katika ubao wa matangazo ya shule ya sekondari Usongwe.

BAADHI ya wazazi wa kata ya Utengule Usongwe, wilaya ya Mbeya Vijijini, wametibua mpango wa kuchangishwa fedha harakaharaka, ili watoto wao waanze kidato cha kwanza kupitia elimu ya watu wazima.

Mpango huo ulikuwa ukiratibiwa na kitengo cha Elimu ya watu wazima mkoa wa Mbeya chini ya Mkufunzi mkazi wa taasisi hiyo Danstan Msamada, kupitia shule ya Sekondari Usongwe iliyopo eneo la Mbalizi.

Baada ya baadhi ya wananchi kushtukia suala hilo, walimpigia simu Diwani wa kata hiyo, Elia Mkono(Chadema), ambaye alianza kufuatili kisha kuitisha mkutano wa wazazi, walimu na Mkufunzi wa taassi hiyo.

Katika kikao hicho kilichofanyika leo katika ukumbi wa shule ya Sekondari Usongwe, wananchi waliuliza maswali 22, ambayo wakati wa kujibiwa, zilitokea zomeazomea kwa kiongozi wa taasisi hiyo na baadhi ya walimu.

Mwananchi Harun Abdalah, aliuliza kuwa iweje baadhi ya watoto wenye wastani wa alama C, wachukuliwe kwenda taasisi ambayo inaendesha elimu katika mfumo usio rasmi?

Benard Tawete, alisema kuwa huo ni mpango wa biashara (dili), kati ya Mkuu wa shule ya Usongwe na taasisi hiyo ili kujipatia fedha kutoka kwa wazazi kwasababu iweje, fomu wazazi wachukue katika shule ya Usongwe kisha wanafunzi wakasome Taasisi iliyopo mbali na shule hiyo?

Wananchi wengi waliulza maswali ambayo, yakawa mwiba kwa baadhi ya viongozi na kushindwa kuyajibu kwa ufasaha kisha kuzomewa.

Afisa Mtendaji wa kata hiyo, Godwin Kaunda, aliamua kujitoa katika zomea zomea hiyo, kwa kuweka wazi kuwa ofisi yake baada ya kulipata jambo hilo aliwakataza wahusika kubandika majina hayo kwenye ofisi yake kabla wananchi hawajaelimishwa, lakini alishangaa kuona kuambiwa majina hayo yamebandikwa siku chache shuleni na wazazi kuanza kuchukua fomu.

Ukweli huo ulimwondoa katika doa la kuwa mmoja wa washiriki wa jambo hilo ambalo wananchi walisema kuwa awali walilaghaiwa kuwa watoto wao walikuwa wamefaulu kwenda huko na kutakiwa kulipa karo ya Tsh.200,000/=, na michango mingine zikiwemo fedha za madawati Tsh.15,000/=, vitambulisho Tsh. 5,000/=, ulinzi Tsh. 5,000 na fomu Tsh.5,000/=.

Diwani wa kata hiyo, Elia Mkono ambaye pia ni mwenyekiti wa Kijiji cha Mbalizi, aliwaambia wananchi kuwa yeye hawezi kuwaambia wananchi kuwa huko wanakotakiwa wawapeleke watoto wao ni kuzuri au kubaya.

“Jaribuni kupima wenyewe, kwasababu hata mimi nimepata takwimu za wanafunzi ambao majina yao yameenda huko Taasisi baada ya kupambana na kulazimisha kupata taarifa zaidi!’’ alisema Mkono na kuanza kufafanua zaidi.

Alisema mpaka sasa, wanafunzi waliofaulu na kuchaguliwa kujiunga na shule mbili za serikali zilizopo katika kata yake katika mfumo maalum ni 601.

Lakini alisema kuwa wakati shule hizo mbili zina idadi ya wanafunzi 601, Taasisi ya elimu ya watu wazima kwa shule moja, imechagua majina ya wanafunzi 493, hali ambayo alisema wazazi wenyewe wachanganue kama wakiwapeleka watoto wao huko watapata elimu bora au la.

Akijibu maswali zaidi, Mkufunzi mkazi wa elimu ya watu wazima huku mara kadhaa akiomba radhi, alisema kuwa taasisi hiyo ni ya serikali na majina hayo ameyatoa serikalini kwa wanafunzi ambao wana wastani wa alama D.

‘’Kama mnaona mfumo huu hamna imani nao msiwalete wanafunzi lakini kwa wale walioelewa wawalete wanafunzi ambao watafundishwa na walimu kutoka hapa shule ya Sekondari Usongwe, wakitoka kufundisha wanafunzi waliopo kwenye mfumo maalum’’ alisema Msamada.

Baadhi ya walimu wa shule ya Usongwe waliozungumza na Mwandishi wa habari hizi shuleni hapo kwa makubaliano ya kutoandika majina yao, walisema wanashindwa kwenda kufundisha vema katika taasisi ya elimu ya watu wazima kutokana na kupewa ujira mdogo.

Waliutaja ujira huo wanaolipwa kwa mwezi kuwa ni Tsh.20,000/= wakati hata wasipokwenda huko hakuna sheria inayowabana kwasababu mikataba yao ya kazi haielezi kuwa watakuwa na kazi nyingine ya kufundisha au kujitolea katika taasisi hiyo.

Kwa takwimu zilizopatikana, zinaonesha kuwa, katika kata hiyo, kuna shule za msingi 13 ambazo zimetoa wanafunzi wa elimu katika mfumo rasmi kama ifatavyo na wanafunzi kwenye mabano.

Shule ya Msingi, Mlima reli(87), Jitegemee(60), Mapambano(35), Mtakuja(100), Mkombozi(117), Mbalizi Moja(96), Onicar(37), Utengule(41), Itimba(5), Idugumbi(6), Iwala(10), Igunga(6) na Iwanga(1).

Taasisi ya elimu ya watu wazima imejinyakulia Mlimareli(47), Jitegemee(124), Mapambano(35), Mtakuja(54), Mkombozi(46), Mbalizi Moja(31), Iwanga(32), Itimba(30), Igunga(28), Iwala(23), Utengule(18) na Idugumbi(25).

Mkutano huo uliisha huku baadhi ya viongozi akiwemo WEO, kuondoka na makubaliano yalikuwa hakuna ulazima wa kumlazimisha mzazi kuchukua fomu ili wanafunzi hao waende kusoma kwenye mfumo huo ambao siyo rasmi na ziachwe propaganda kuwa watoto hao wamefaulu kwenda huko.
 
Chanzo; kalulunga.com

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

NAIBU WAZIRI WA KILIMO MHE MWANJELWA AMUAGIZA MRAJIS KUFANYA UCHUNGUZI SACCOS YA MADIBIRA-MBARALI NDANI YA SIKU 14

Naibu Waziri wa Wizara ya Kilimo, Mhe Mary Mwanjelwa akisisitiza jambo wakati akizungumza na Viongozi mbalimbali wa Mkoa na kamati ya uli...